Friday, August 21, 2015

MASHIRIKA ya UN yaaadhimisha miaka 70 kwa kupanda miti 2,000


Balozi wa Ireland akipanda mti

MASHIRIKA ya Umoja wa Mataifa yaliyopo nchini yameadhimisha miaka 70 ya kuundwa kwa umoja huo kwa kupanda zaidi ya 2000 katika miteremko ya mlima Kilimanjaro.


Kazi ya kupanda miti ilifanywa na wafanyakazi wa Umoja wa Mataifa na wadau wao ikiwemo serikali ya Tanzania pamoja na wanakijiji.

Kazi ya kupanda miti iliongozwa na Mratibu Mkazi wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi wa Shirika la Maendeleo (UNDP) nchini, Alvaro Rodriguez akishirikiana na Mwakilishi wa Makamu wa Rais, Waziri wa Nchi ofisi ya Makamu wa Rais anayeshughulikia Mazingira, Binilith Mahenge.

Shughuli hizo za kupanda miti zilifanyika katika kijiji cha Maruwa.

Akizungumza wakati wa shughuli hiyo Waziri Mahenge alisema kwamba amefurahishwa na hatua iliyochukuliwa na Umoja wa Mataifa ya kuadhimisha miaka 70 kwa kuwakumbusha washirika wao wa maendeleo suala la mazingira.

“Ni kawaida kuadhimisha kuundwa kwa Umoja wa Mataifa Oktoba 24 kila mwaka. Mwaka huu ni tofauti na zaidi ya tofauti umekuwa maalumu kwa namna yake kwa kuwa tunaadhimisha miaka 70 ya uwapo wa Umoja wa Mataifa.” alisema Waziri Mahenge.
Kwa upande wake balozi wa Ulaya alisema upandaji miti katika mteremko wa mlima Kilimanjaro kuadhimisha miaka 70 ya Umoja wa Mataifa ni alama muhimu katika mapambano ya wanadamu kulinda mazingira.

Alisema ishara hiyo muhimu inaelekeza Umoja huo na wadau wake wa maendeleo kuchukua tahadhari za kutosha kulinda mazingira na inakwenda sanjari na malengo endelevu ya milennia (SDGs) ambayo yana mada tano za kuangaliwa katika mazingira kuliko yale ya awali ambayo yalikuwa na mada moja tu.

Msemaji wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa, Hoyce Temu alisema kwamba upandaji miti uliofanyika ni moja ya shughuli kadhaa zitakazofanywa na Umoja huo kuadhimisha miaka 70 toka kuanzishwa kwake.

.

No comments:

Post a Comment