IMEELEZWA kuwa Tanzania inapata
hasara ya shilingi bilioni 301 kila mwaka, sawa na bajeti za wizara mbili,
kutokana na wananchi wake zaidi ya milioni tano kutotumia vyoo, na hivyo
kusababisha magonjwa ya milipuko yanayoweza kuzuilika.
Akiwasilisha taarifa ya utafiti uliofanywa na
Benki ya dunia, Meneja Mipango na Uendeshaji wa Mradi wa Usafi wa Mazingira
Tanzania, mhandisi Koronel Kema, amesema kutokuwepo kwa usafi wa mazingira
kunailetea nchi hasara kwa kuyatibu magonjwa yanayotokana na uchafu badala ya
kuyazuia.
Mhandisi Kema amebainisha leo na kusisitiza kuwa
kutokuwepo kwa usafi wa mazingira kunachangia vifo, ambapo inakadiriwa
watanzania zaidi elfu 20 kati yao wakiwemo watoto elfu kumi na nane hupoteza
maisha.
Awali akifungua mafunzo ya uandishi wa habari za
mazingira, Mkuu wa Wilaya ya Bahi Bi. Betty Mkwasa amesema pamoja na wilaya
anayoiongoza kuwepo katika mradi wa ujenzi wa vyoo bora bado serikali wilayani
humo imetenga siku moja ya usafi katika wiki, kabla ya watu kwenda kufanya shughuli
nyingine za maendeleo, baada ya kutambua umuhimu wa kutunza mazingira.
Mradi wa usafi wa mazingira Tanzania (UMATA)
unaosimamiwa na Plan International, unatekelezwa katika wilaya tatu za mkoa wa
Dodoma, ambayo ni Bahi, Kongwa na Chamwino, huku lengo la mradi huo likiwa
kuwahamasisha wananchi kutumia vyoo bora na kujenga tabia ya kunawa mikono,
kabla ya kula na wanapotoka chooni.
-------------------------------------------
MAADHIMISHO ya 17 ya wiki ya Maziwa
kitaifa yamezinduliwa leo mkoani Mara ambapo imeelezwa kuwa kiwango
cha unywaji Maziwa bado ni kidogo ikilinganishwa na kile kilichopendekezwa na
Shirika la Chakula na Afya Duniani.
Mwakilishi wa Kaimu Mkuu wa mkoa wa Mara Bw
Jackson Msome ambaye pia ni Mkuu wa wilaya ya Musoma ameyasema hayo katika
uzinduzi wa maadhimisho ya 17 ya wiki ya Maziwa katika uwanja wa Shule Msingi
Mukendo Manispaa ya Musoma mkoani Mara.
Amesema lengo la Maadhimisho hayo ni kulenga
shughuli za wadau wa Maziwa ingawa kuna changamoto kubwa kwa viwanda vya
usindikaji Maziwa nchini huku akisema kuwa kutokana na uzalishaji kwa sasa
wastani wa unywaji Maziwa kwa mtu ni lita 45 kwa mwaka huku viwango
vilivyopendekezwa na Shirika la WHO na FAO ni kunywa Maziwa lita 200 kwa
mwaka.
Katika Maadhimisho hayo ambayo kilele chake ni
june mosi mwaka huu shirika la taifa la hifadhi ya Jamii NSSF limeendesha
kambi ya upimaji wa afya bure kwa wakazi wa Mkoa wa Mara ambapo litaendesha
zoezi hilo kwa siku tatu na baadae kuelekea katika mikoa ya shinyanga, Geita na
Kagera
No comments:
Post a Comment