JUMUIYA ya Ulaya (EU)
imetiliana saini na mashirika ya Umoja wa Mataifa yaliopo nchini Tanzania
yanayofanya kazi kama shirika moja (One UN) ruzuku ya Euro 200,000 (sawa na Sh.
milioni 478) kwa ajili ya shughuli za maendeleo zitakazonufaisha wananchi wa
Tanzania.
Shughuli ya utiaji saini ilifanywa na Mratibu
wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa nchini Tanzania, Alvaro Rodriguez na Balozi wa
EU nchini, , Filiberto Ceriani Sebregondi katika Ofisi za EU jijini Dar es
Salaam na kushuhudiwa na wakuu wa mashirika ya UN na wa EU.
Ruzuku hiyo imelenga kusaidia miradi ya pamoja
ya EU na UN ya mawasiliano, uragibishi, uimarishaji wa ufuatiliaji na uwazi.
Maeneo hayo ni muhimu kwa shughuli za EU na Umoja wa Mataifa nchini Tanzania.
Akisisitiza mchango wake kwa One UN, balozi wa
EU, Filiberto Ceriani Sebregondi, alisema Tanzania imefanikiwa kutengeneza
mfano bora wa namna Mashirika ya Umoja wa Mataifa yanavyoweza kufanya kazi kama
taasisi moja katika kuboresha maisha ya watu wa nchi yake.
EU nchini Tanzania imekuwa na ushirikiano
katika program kadha na mashirika ya Umoja wa Mataifa hasa IOM, Unicef, UNDP,
UNODC, UNHCR, Fao, Unesco, Ifad, UN Women na WFP.
Kwa sasa EU imeshatoa Euro milioni 43 kwa
ajili ya miradi mbalimbali inayotekelezwa na mashirika ya Umoja wa Mataifa
Tanzania.

No comments:
Post a Comment