Tuesday, January 5, 2016

BURUNDI haitoshiriki mazungumzo ya amani kesho

SERIKALI ya Burundi imesema haitashiriki duru ya pili ya mazungumzo ya amani na upinzani yanayotazamiwa kuendelea kesho mjini Arusha nchini Tanzania.


Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Burundi, Joseph Bangurambona, amesema upande wao hautashiriki kikao cha kesho na cha Januari 16 cha kujaribu kuutafutia ufumbuzi mzozo wa kisiasa katika nchi hiyo ya Afrika Mashariki.
Bangurambona amesema pande husika hazijakubaliana kuhusu tarehe kamili ya kuendelea na mazungumzo hayo. Kamisheni ya Umoja wa Afrika imetishia kuziwekea vikwazo pande hasimu za nchi hiyo ya Afrika Mashariki, iwapo wawakilishi wao hawatashiriki mazungumzo ya amani mwezi ujao.

Duru ya kwanza ya mazunguzo hayo ilifanyika mjini Entebbe nchini Uganda chini ya usimamizi wa Rais Yoweri Museveni. Umoja wa Mataifa umezitaka pande hasimu nchini Burundi kufikia makubaliano kuhusiana na mzozo wa kisiasa unaoikabili nchi hiyo ambao umepelekea kutokea mauaji ya kiholela.

Burundi ilitumbukia katika machafuko na ghasia za ndani baada ya Pierre Nkurunziza kutangaza nia yake ya kuwania tena kiti cha urais kwa kipindi cha tatu mfululizo hapo Aprili mwaka huu. Wapinzani wanasema kuwa, uamuzi wa kiongozi huyo ulikiuka katiba ya nchi na makubaliano ya amani ya Arusha yaliyohitimisha rasmi vita vya ndani vya Burundi.







No comments:

Post a Comment