KUNDI la Boko Haram limewakamata mateka zaidi ya wanawake 60 katika vijiji vya Kumanza, Yaga, Dagu na Damboa katika jimbo la Borno, lililoko kaskazini mashariki mwa Nigeria.
Haji Khalil kiongozi wa kieneo amesema kuwa, wanakijiji kadhaa wameuawa kwenye shambulio hilo, na wengine wamekimbilia maeneo mengine kutafuta hifadhi.Khalil amesisitiza kuwa, zaidi ya wanawake 60 wametekwa mateka na wanamgambo waliokuwa na silaha wa kundi hilo. Tukio hilo linatokea katika hali ambayo, serikali ya Nigeria bado inaendeleza juhudi za kuwakomboa wanafunzi wasichana zaidi ya 250 wanaoshikiliwa na kundi la Boko Haram. Ambapo mpaka sasa serikali kuu ya Nigeria haijatoa taarifa zozote rasmi kuhusiana na shambulio hilo lakini mashuhuda, viongozi wa kieneo na duru za habari katika jimbo la Borno zimeeleza kwamba, wanamgambo wa kundi la Boko Haram waliharibu nyumba kadhaa za wanavijiji katika eneo hilo.
Mwezi Aprili mwaka huu kundi hilo lilishambulia shule ya sekondari ya wasichana ya Chibok iliyoko jimbo la Borno na kuwakamata mateka wanafunzi 276 ambapo 50 kati yao walifanikiwa kutoroka mikononi mwa wanamgambo hao.

No comments:
Post a Comment