Thursday, March 24, 2016

Dr Haji Mponda atoa vifaa vyenye thamani ya shilingi milioni 20 jimboni kwake

Mbunge wa Malinyi  Dk Haji Mponda 
MBUNGE wa jimbo la Malinyi mkoani Morogoro Dk Haji Mponda amemwaga vifaa mbalimbali vya thamani ya shilingi mil.20 ikiwemo mashine ya kufulia nguo,matanki mawili yenye uwezo wa kuhifadhi lita 5,000 sambamba na kukiunganishia umeme kituo cha Afya Mtimbira wilaya mpya ya Malinyi.


Dk Mponda aliamua kumwaga vifaa hivyo baada ya kutoridhishwa na hali yake kutokana na kuchakaa baada ya kujionea alipo alipokitembelea juzi.

Akizungumza na watumishi wa kituo hicho,Dk Mponda aliiomba serikali itafute njia nyingine ya kukisaidia kituo hicho cha afya ikiwemo kuondoa tatizo la upungufu wa watumishi na  madawa wakati mchakato wa kupandisha hadhi kutoka kituo cha afya kwenda hospitali ukisubiriwa.

Alisema kituo hicho kina changamoto nyingi na ni bahati mbaya  katika jimbo zima na wilaya ya Malinyi kituo kinachofanya kazi ni kimoja tu na nyingine ni hospitali ya binafsi ya Lugala inayomilikiwa na kanisa la kilutheri.

Kwa mujibu wa Mbunge huyo changamoto zinazokikabili kituo hicho ni pamoja  na upungufu wa dawa na watumishi wachache na kusema kuwa anashindwa kuzitatua changamoto hizo tokana na sera kuweka mipaka hasa kituo cha afya kuwa na ikama ya watumishi na mgao wake wa dawa.

Ameshangazwa na sera hiyo na kutolea mfano kuwa  ndani ya miezi mitatu kituo hicho kinapata mgao wa shilingi milioni 2 za madawa wakati hospitali ya wilaya Mahenge inapata shilingi milioni 20 ya mgao huo ndani ya miezi hiyo mitatu huku kituo hicho kinahudumia wagonjwa wengi kuliko hospitali ya wilaya.

Ametolea mfano kuwa kila mwezi kituo hicho kinapokea akinamama 150 wanaokuja kujifungua wakati hospitali ya wilaya hupokea akinamama 100 tu hivyo kuiomba serikali kusaidia  wilaya hiyo kuwa mpya.



No comments:

Post a Comment