![]() |
| Kiwanda cha 21st century |
MOTO mkubwa
umezuka Kiwanda cha nguo cha 21st Century kilichopo Kihonda
Manispaa ya Morogoro na kuteketeza vitu mbalimbali ikiwemo baadhi ya mitambo ya
kuzalisha nguo na malighafi kiwandani hapo.
Meneja uzalishaji wa kiwanda hicho Clement Munisi aliwaambia wanahabari mjini hapa kuwamoto huo ulizuka majira ya saa 12.00 asubuhi juzi katika mashine moja ya kusuka vitambaa ikitoa cheche ambapo wafanyakazi waliokuwa zamu walipojaribu kuuzima kwa kutumia kifaa maalumu cha kuzima moto (Fire extinguisher ) ilishindikana.
Munisi alisema kuwa moto huo uliendelea kuenea katika vyumba vingine ndani ya kiwanda hicho na kusababisha baadhi ya nguo zilizokuwa zikiendelea kusukwa katika mitambo hiyo kuteketea vibaya na hasara yake haijafahamika mpaka sasa..
Kamanda wa kikosi cha zimamoto Mkoa wa Morogoro Ramadhani Pilipili alisema kuwa licha ya kuwahi kufika mapema katika eneo la tukio na juhudi za kuuzima moto zikiendelea lakini bado miundombinu ya kiwanda hicho bado imekuwa ni kikwazo .
Kwa upande mwingine Kamanda huyo alitoa wito kwa uongozi wa kiwanda kuhakikisha wanaweka miundombinu ya mabomba juu ya paa ili ikitokea tena tatizo kama hili iwe rahisi kushughulikiwa ikiwemo uzimaji moto.
Afisa Mazingira wa kiwanda hicho Anna Gerevas alisema kuwa
wafanyakazi wa kiwanda hicho wako hatarini kukosa ajira kutokana na uharibifu
uliosababishwa na moto huo jambo linaloweza kupelekea kiwanda hicho
kufungwa kwa muda na wafanyakazi kubaki majumbani.
hata hivyo baadhi ya wafanyakazi waliwabainishia wanahabari kwa
sharti la kutotajwa majina yao wakisema kuwa mashine hizo zimekuwa zikitoa
cheche kwa muda mrefu wakibainisha kuwa hiyo ni mara ya tatu kutaka kulipuka na
kuzimwa mapema.

No comments:
Post a Comment