RAISI wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho
Kikwete amesema kuwa ni utovu wa nidhamu na ukosefu wa adabu kwa baadhi ya
Watanzania kuwatukana, kuwadhihaki na kuwakejeli Waanzilishi wa Taifa la
Tanzania, Hayati Julius Nyerere na Hayati Sheikh Abeid Amaan Karume.
Aidha, Rais Kikwete amesema kuwa viongozi hao wawili wameifanyia
Tanzania mambo mengi, mambo makubwa na mambo ya kihistoria kiasi cha kwamba
Watanzania wanao wajibu wa kudumisha na kuenzi heshima yao kwa namna ya kudumu.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo na Kurugenzi ya Mawasiliano
ya Rais,Ikulu,jijini Dar es salaam,Kauli hiyo ameitoa wakati akizungumza
na Wahariri wa baadhi ya vyombo vya habari usiku wa jana, Jumatano, Aprili 16
katika mahojiano maalum ya kuadhimisha Miaka 50 ya Muungano.
Rais Kikwete amesisitiza kuwa ni ukosefu wa adabu kwa yoyote
kumshutumu mtu aliyejitolea kiasi hicho ili kubadilisha mfumo dhalimu na
kujenga maisha na mazingira ya maisha bora kwa wengi.
Rais Kikwete ametoa msimamo huo baada ya kuwa ameulizwa kuhusu
matusi, kejeli, dhihaki ambazo zimekuwa zinaonyeshwa na wajumbe wachache wa
Bunge Maalum la Katiba juu ya waasisi hao wa Tanzania na Wabunifu Wakuu wa
Muungano wa Tanzania.
No comments:
Post a Comment