UONGOZI
wa kampuni ya kusindika Tumbaku ya Alliance One Tanzania Limited ya mjini
Morogoro umetoa msaada wa vyakula wenye thamani ya shilingi milioni tano kwa
ajili ya waathirika wa mafuriko wa Wilaya ya Morogoro.
Akizungumza katika makabidhiano ya msaada
huo uliotolewa jana mbele ya mkuu wa Wilaya ya Morogoro Bwana Saidi Amanzi,meneja
mahusiano wa kampuni hiyo,Bwana Hamisi Liana,amesema kuwa kampuni hiyo imepokea
kwa masikitiko makubwa taarifa ya kuwa zaidi ya kaya 1396 zenye jumla ya watu
6986 ndani ya wilaya hiyo zimeathirika na mafuriko hayo.
Aidha Bwana Liana amesema kuwa mafuriko ni
janga ambalo hutokea mahali popote na wakati wowote hususani wakati wa
mvua nyingi kama ilivyotokea kwa wakazi hao wa wilaya ya Morogoro na
kusababisha hekta zipatazo 2778 za mazao mbalimbali kuharibika.
Sambamba na hilo amesema kuwa kampuni ya
Alliance One itaendelea kushirikiana na uongozi wa serikali wakati wote
itakapohitajika kufanya hivyo,huku akiwaomba watanzania na makampuni mbalimbali
kushiriki katika kuwasaidia watu hao waliopatwa na janga hilo la mafuriko.
Msaada wa vyakula uliotolewa ni mifuko 100
ya unga wa sembe yenye kilo 25 kila mmoja,kilo 1000 za maharage pamoja na lita
200 za mafuta ya kupikia.
No comments:
Post a Comment