Wednesday, May 28, 2014

MWAMKO mdogo wa jamii katika kuchangia damu ni chanzo cha ukosefu wa damu katika benki za damu



IMEELEZWA  kuwa mwamko mdogo katika uchangiaji damu kwa mamlaka zinazohusika na ukusanyaji wa damu salama nchini ndio chanzo kikubwa cha ukosefu wa damu katika benki za damu kwenye hospitali mbalimbali nchini,hali inayochangia vifo vingi vingi vya kinamama wakati wa kujifungua.

Hayo yamesemwa jana jijini Dar es salaam na mkurugenzi wa tiba ,wa wizara ya Afya na ustawi wa jamii Dk MAGRETH MHANDO, katika hotuba iliyosomwa kwa niaba yake na Dk.PAULO MHAME wakati wa uzinduzi wa warsha ya siku moja ya viongozi wa madhehebu mbalimbali ya dini pamoja na maofisa kutoka serikalini,waandishi wa habari na wadau wa damu salama.

Amesema hali hiyo inatokana na wananchi kutopatiwa elimu ya kutosha juu ya uchangiaji wa damu kwa kukidhi mahitaji yanayosababishwa na matukio mbalimbali ndani ya jamii huku baadhi ya wanajamii wakiamini kuwa kwa kufanya hivyo kuna kitu wanachopoteza.

Viongozi wa dini walioshiriki katika warsha hiyo wametoa maoni yao juu ya namna bora ya kupata wananchi wengi kuchangia damu na wamekemea tabia ya baadhi ya wafanyakazi wa maabara kuuza damu zinazochangwa kwa manufaa yao binafsi.

No comments:

Post a Comment