RAISI wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ameitaka sekta
binafsi kujihusisha zaidi katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa UKIMWI kwa
sababu ugonjwa huo unaathiri uchumi na biashara na kuongeza mzigo wa gharama za
uzalishaji wa makampuni hayo.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais Kikwete amesema kuwa pamoja na kwamba Tanzania imekuwa inapata michango mikubwa ya kupambana na UKIMWI kutoka kwa washirika wake wa maendeleo, bado jukumu la msingi la kupambana na ugonjwa huo nchini ni la Watanzania wenyewe.
Pia, Rais Kikwete amewakumbusha Watanzania kuwa UKIMWI hauna tiba ya kisayansi ama tiba mbadala ya waganga wa jadi ama wapiga ramli kama baadhi ya Watanzania wanavyopenda kujiaminisha.
Rais Kikwete alikuwa anazungumza hayo usiku wa kuamkia, Jumamosi,wakati alipokuwa Mgeni Rasmi katika hafla ya uzinduzi wa uchangishaji fedha za kupanda Mlima Kilimanjaro kwa ajili ya mapambano ya UKIMWI kwa mwaka huu wa 2014 kwenye Hoteli ya Regency jijini Dar es Salaam.
Katika shughuli ya usiku huo, Rais
Kikwete alitoa hundi ya shilingi milioni 700 kwa taasisi mbali mbali kutokana
na fedha zilizokusanywa mwaka jana chini ya mpango huo wa Kili Challenge.
No comments:
Post a Comment