Friday, May 9, 2014

TANZANIA yafanya vizuri zaidi barani Afrika katika uandikishaji wa watoto kuanza shule



MJUMBE  Maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu Elimu ya Kimataifa  na Waziri Mkuu wa zamani wa Uingereza,bwana Gordon Brown amesema kuwa Tanzania imefanya vizuri zaidi kuliko nchi nyingine yoyote ya  Afrika katika uandikishaji wa watoto kuanza shule.

Bwana Brown amekutana na Rais Kikwete kwenye Hoteli ya Hilton mjini Abuja ambako wote wawili wanakaa kwa ajili ya kuhudhuria Kongamano la Uchumi Duniani – kwa Bara la Afrika lilioanza jana katika mji mkuu wa Nigeria Abuja.
Kwa sababu hiyo na kwa sababu ya mafaniko hayo Brown amesema kuwa Umoja wa Mataifa na Taasisi zake na  nyingine za kimataifa ziko tayari kuisaidia Tanzania kufikia lengo la kusajili watoto wote kwa asilimia 100 ya watoto  wanaotakiwa kuingia shule katika muda wa uongozi wa Rais Kikwete na kabla hajaondoka madarakani mwishoni mwa mwaka ujao.
.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na kurugenzi ya mawasiliano ya Rais Ikulu,Rais Kikwete pia amekutana na kufanya mazungumzo na  Bwana Mark Suzman, Mkurugenzi wa Sera na Mipango wa Taasisi ya Bill and Melinda Gates ya Marekani. Aidha, Rais amekutana na kufanya mazunguzo na Bwana Sunnil Bharti Mittal, Mwenyekiti wa Kampuni ya kimataifa ya simu ya Airtel duniani.

No comments:

Post a Comment