Sunday, June 22, 2014

VYAMA vikuu vya Upinzani vyasusia uchaguzi nchini Mauritania


RAIS wa Mauritania  Mohammad Oud Abdulaziz akipiga kura hapo jana
WANANCHI  wa Mauritania wamepiga kura katika uchaguzi tata wa rais ambapo vyama vikuu vya upinzani vimesusia huku rais wa sasa Mohammad Ould Abdel Aziz akitazamiwa kupata ushindi.

\
Abdel Aziz ambaye ni muitifaki wa nchi za Magharibi katika kile kinachoodaiwa kuwa ni vita dhidi ya ugaidi Afrika Magharibi anatazamia kuimarisha mamlaka yake kwa uchaguzi huo.

Katika uchaguzi huo wa jana Jumamosi, kulikuwa na wapiga kura wachache katika mitaa ya matajiri katika mji mkuu Nouakchott huku idadi kubwa wakijitokeza katika vitongoji vya mji huo. Duru ya pili ya uchaguzi itafanyika July 5 iwapo hakutapatikana mshindi.

Wapinzani pia mwaka jana walisusia uchaguzi wa bunge wakisema waandalizi wanapendelea upande moja. Mazungumzo ya kujaribu kuwashawishi wapinzani washiriki katika uchaguzi wa jana yalifeli mwezi Aprili na hivyo kumuacha Abdel Aziz bila mpinzani mkubwa. Karibu watu milioni 1.3 wametimiza masharti ya kupiga kura nchini Mauritania.

Nchi hiyo iliyo baina ya magharibi na kaskazini mwa Afrika ina utajiri mkubwa wa madini ya shaba na dhahabu na inaaminika kuwa na akiba kubwa ya mafuta na gesi.




No comments:

Post a Comment