Friday, March 13, 2015

MGOGORO wa Kihansi na wananchi wa Mlimba wapatiwa ufumbuzi



Mtambo wa Tanesco  Kihansi, Kilombero, Morogoro

HATIMAE mgogoro wa ardhi uliodumu kwa karibu miaka 20 kati ya wananchi wa Mlimba na shirika la umeme nchini(Tanesco) tawi la Kihansi umetatuliwa na halmashauri ya wilaya ya Kilombero, mkoani Morogoro.


Katika mkutano wa mapatano pande hizo mbili,kaimu mkurugenzi wa halmashauri hiyo Jackson Mpankuli alisema wameamua kuingilia kati kupata ukweli na kumaliza tatizo hilo.

Alisema hatua baada ya mazungumzo hayo ni wananchi kupitia kamati waliyoiunda kusimamia mgogoro huo kwa kuanza upya maombi ya ardhi wakieleza mahitaji yao toka katika eneo hilo lenye ukubwa wa hekta 28 kwakua ni eneo halali la Tanesco.

Kaimu mkurugenzi huyo alisema kuwa wao kama halmashauri watashirikiana na wananchi katika maombi hayo ili kuhakikisha eneo linapatikana na shughuli za maendeleo zinafanyika eneo moja huku eneo lingine likibaki kwa Tanesco Kihansi.

Awali mwenyekiti mstaafu kijijini hapo Benard Namhongoma alitoa histora fupi ya shirika hilo kupata eneo hilo akisema kijijini hapo mwaka 1994 akisema walifuata hatua zote za kisheria wakati huo na waliokutwa eneo hilo walilipwa fidia.

Namhongoma alisema wao waliridhia na kuomba wananchi waliokuwepo eneo hilo ambao walikuwa wakiliendeleza kwa shughuli za makazi na kilimo kutoka na kuwapisha Tanesco na shirika lilianza ujenzi wa hospitali ambayo ipo hadi leo.

Aliongeza kuwa Rais mstaafu Benjamin Mkapa alipoagiza hospitali hiyo irudishwe kwa wananchi shirika lilikubali na lilibaki eneo hilo kwa ajili ya nyumba za watumishi na sio kweli kwamba eneo hilo waliwapa Tanesco kwa ajili ya makazi binafsi ya watumishi.

Kwa upande wake meneja wa Tanesco Kihansi Pakaya Mtemakaye alisema shirika hilo wanamiliki eneo hilo kihalali na waliwalipa watu wote waliowakuta eneo hilo kwa kufuata sheria ya mwaka ule na ofisi yake haina lalamiko la madai na anashangaa kusikia kuwa kuna watu wamepewa eneo hilo.

Nae afisa ardhi na maliasili wa wilaya Sakurani Mushi alisema wakati serikali inaomba eneo hilo sheria iliyotumika ni ya mwaka 1923 na fidia iliyotumika ni ya mwaka 1967 na malipo yalifanyika bila malalamiko kuhusu fidia na Tanesco wana hati miliki halali ya eneo hilo.

Mushi alisema wakati Tanesco wanaomba eneo hilo waliomba kwa ajili ya nyumba za wafanyakazi,viwanja vya michezo na hospitali na kwa sasa wamejipanga upya kwa kutaka kujenga makazi yao na hawana kosa kwa kujipangia matumizi katika eneo lao.






























https://ssl.gstatic.com/ui/v1/icons/mail/no_photo.png

No comments:

Post a Comment