Saturday, May 21, 2016

MKAPA ateuliwa kuongoza mazungumzo kuhusu mgogoro wa Burundi

Rais  wa awamu ya tatu wa Tanzania Benjamini Mkapa akiwa na Rais wa Tanzania John Pombe Magufuli 

RAIS Mstaafu wa Awamu ya Tatu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Benjamin Mkapa, ameteuliwa kuongoza mazungumzo kuhusu mgogoro wa Burundi ikiwa ni jitihada za viongozi wa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki kataka kuleta amani ya kudumu nchini humo.

Mkapa, aliyeteuliwa na Mkutano wa 17 wa wakuu wa nchi wa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki atakuwa kiongozi wa timu ya usuluhishi wa mgogoro wa Burundi katika kikao kitakachofanyika kuanzia kesho 21 hadi Mei 24 mwaka huu.

Kikao hicho cha usuluhishi kinatarajiwa kufanyika katika ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa (AICC) jijini Arusha. Taarifa zilizopatikana zilieleza kwamba pande zote zinazohusika na mgogoro huo zitashiriki.

Aidha, Mkutano huo wa 17 wa wakuu wa nchi wa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki ulifafanua  kuwa Rais wa Uganda, Yoweri Museveni, ataendelea kuwa msuluhishi wa kudumu kutoka jumuiya hiyo.

Serikali ya Burundi ilikubali kufanyika usuluhishi huo na iko tayari kushiriki katika mazungumzo ya amani yanayofanywa na viongozi wa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki yakihusisha wadau wote wa siasa nchini Burundi ikiwa ni jitihada za kuumaliza mgogoro wa kisiasa unaoendelea nchini humo













No comments:

Post a Comment